Na Happiness Katabazi
SHAHIDI wa pili katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7, inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake, Betha Msoka (44), ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam kuwa hakuna mahali popote panapomlazimisha Waziri wa Fedha kuomba ushauri wa kutoa msamaha wa kodi Mamlaka ya Mapato nchini (TRA).
Sambamba na hilo, pia Msoka ambaye ni mwanasheria kitaaluma, amesisitiza kuwa hana ushahidi kwamba Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali haikushirikishwa kwenye mchakato wa kuitafuta Kampuni ya ukaguzi wa madini ya Alex Stewart Government Business Corporation.
Wakati shahidi huyo akitoa maelezo hayo, kwa mujibu wa hati ya mashitaka inasomeka kuwa washitakiwa hao wanakabiliwa na kosa la kukaidi ushauri wa TRA uliotaka kampuni hiyo isipewe msamaha wa kodi, lakini kwa nafasi zao waliamua kutoa msamaha huo.
Shahidi huyo wa upande wa mashitaka alitoa madai hayo jana mbele ya jopo la mahakimu wakazi; John Utamwa, Saul Kinemela na Sam Rumanyika wakati akihojiwa na mawakili wa utetezi; Hurbet Nyange, Peter Swai, Elias Msuya, Cuthbet Tenga na Profesa Shahidi.
Yafuatayo ni mahojiano baina ya mawakili hao na shahidi huyo:
Wakili: Ulishawahi kufanya kazi katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kama Mwanasheria wa Serikali?
Shahidi: Ndiyo.
Wakili: Ulifanya kazi katika ofisi hiyo kwa muda gani?
Shahidi: Sikumbuki ila nilifanya kazi kwa muda mfupi kwani nilipata barua toka Ofisi ya Utumishi ikiniarifu nahamishiwa Wizara ya Fedha.
Wakili: Hiyo barua ya Utumishi ilikuwa ni ya kukubadilisha kazi au kituo cha kazi?
Shahidi: Kituo cha kazi.
Wakili: Unayo hiyo barua inayokuonyesha umebadilishiwa kazi?
Shahidi: Sina.
Wakili: Tangu 1992 ulipohamishiwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, uliwahi kurudi katika ofisi hiyo kufanya kazi za ofisi hiyo?
Shahidi: Sikuwahi kurudi kwa sababu niliajiriwa na Wizara ya Fedha.
Wakili: Baada ya kutoka katika ofisi ya AG uliwahi kuwa na access ya majalada ya AG?
Shahidi: Sikuwahi kuwa na access ya kushika majalada ya ofisi hiyo.
Wakili: Je, nitakosea kama wewe ukiwa mtumishi wa serikali kama wakili wa serikali, ulikuwa ni daraja kati ya Wizara ya Fedha na ofisi ya AG?
Shahidi: Kuna masuala ambayo ofisi hizo mbili zilikuwa zikishirikiana.
Wakili: Nitakuwa sahihi nikisema masuala ya kisheria mnayoshirikiana na AG, ni Wizara ya Fedha ilikuwa inahusika moja kwa moja?
Shahidi: Mengi ni yale yaliyokuwa yanahusu Wizara ya Fedha moja kwa moja na mengine ambayo yana commontiment na wizara.
Wakili: Ulisema uliitwa BoT kujadili rasimu ya mkataba wa Alex Stewart, na ulibaini vipengele viwili vya kodi na ada, kipi kilikuwa kinahusu wizara yako?
Shahidi: Kipengele cha kodi kilikuwa kinahusu Wizara ya Fedha.
Wakili: Kipengele cha ada wewe akikukusumbua kama mwanasheria wa Wizara ya Fedha?
Shahidi: Ili msamaha wa kodi utolewe, ni lazima Waziri wa Fedha atoe idhini.
Wakili: Je, uliwasiliana na ofisi ya AG kuhusu hicho kipengele cha kodi?
Shahidi: Hatukuwasiliana na AG.
Wakili: Hivi Mramba, Yona na Mgonja wakati wakiwa na nyadhifa walikuwa ni wanasheria?
Shahidi: Hawakuwa na hadi sasa hawana taaluma ya sheria.
Wakili:Juzi uliieleza mahakama hii kwamba tangu uondoke ofisi ya AG ujawahi kurudi kufanyakazi hapo na nikakuuliza unasema uongo ,ukakataa.Kama unakumbuka dokezo la aliyekuwa Waziri wa Nishati(Yona)alilomwandikia Rais Benjamin Mkapa la Mei 11 mwaka 2003 linasomeka “Baada ya kukubali dokezo langu la Machi 3 mwaka 2003 kuhusu umuhimu wa kuanzisha ukaguzi wa dhahabu inayochimbwa na kuuzwa nchi za nje ,majadiliano kati ya Wizaya Nishati,Fedha,BoT na AG yanaenda vizuri’.Nikikwambia Wizara ya Nishati ilikuwa inawasiliana na na AG utasemaje?
Shahidi:Siwezi kujua.
Wakili:Kwahiyo wewe ulikwenda kwenye timu ya majadilio ya rasimu ya mkataba kama mwanasheria wa umma kwani sijakusikia wewe kama unataaluma ya uchumi?
Shahidi:Ndiyo nilikwenda kama mwanasheria.
Wakili:Wewe mwenyewe ulisema ulikuwa ni daraja kati ya Wizara ya Fedha na AG ,wewe uliona kuna haja katika timu hiyo kuletwa mwanasheria toka ofisi ya AG?
Shahidi:Watakuja watu wa ofisi ya AG watasema wenyewe.
Wakili:Una uhakika kama Wizara ya Nishati na Madini haikutafuta ushauri wa AG katika mchakato mzima wa kutafuta kampuni hiyo?
Shahidi:Sina uhakika.
Wakili;Jana ulisema uliandika barua TRA kuomba ushauri kuhusu kipengele cha msamaha wa kodi wa kampuni hiyo ,ebu ionyeshe mahakama hiyo barua?
Shahidi:Sina.
Wakili:Hiyo barua uliyoiandikia TRA kuhusu kipengele cha msamaha wa kodi , inamuweka Mramba kwenye nafasi nzuri.
Shahidi:Ndiyo inamuweka kwenye nafasi nzuri katika kutoa msamaha wa kodi.
Wakili: Una weza kujua ni kwanini upande wa mashitaka umeshindwa kukupa hiyo barua ili uitoe mahakamani kama kielelezo?
Shahidi:Sijui.
Wakili:Nikikwambia upande wa mashitaka umeiacha hiyo barua makusudi ili kumkandamiza mshitakiwa wa kwanza(Mramba)?
Shahidi:Sijui.
Wakili:Ulisema wizara ya Fedha inapotengeza matangazo ya serikali(government Notice) ni kwanini inashirikiana na ofisi ya AG?
Shahidi:Kwasababu matangazo hayo ya serikali ni nyaraka za kisheria.
Wakili:Je Gorvement Notice yakiakikiwa na AG halafu yakasainiwa na waziri wa Fedha, Je waziri akasini matangazo hayo ya serikali,kiongozi huyo anashtahili kulaumiwa?
Shahidi:Hastahili kulaumiwa.
Wakili: Ulisema ofisi ya AG haikuwa na mwakilishi kwenye timu yenu?
Shahidi:Ndiyo.
Wakili:Je hukumaanisha mchakato mzima haukurikisha ofisi ya AG?
Shahidi:Sikumaanisha hivyo.
Wakili:Utakubaliana namimi kwamba mchakato mzima ulishirikisha ofisi ya AG?
Shahidi:Sina hakika na hilo.
Wakili:Una fahamu kuwa Mei 2 mwaka 2003,AG alijibu barua ya Yona aliyomwandikia Machi 3 mwaka 2003?
Shahidi:Sifahamu.
Wakili:Nikikwambia barua hiyo ya AG ipo unaweza kubisha kwani?
Shahidi:Siwezi kubisha.
Wakili:Unaweza kutoa ushahidi kwamba hakukuwepo mawasiliano kati ya Wizara ya Nishati na ofisi ya AG katika mchakato wa kutafuta kampuni hiyo ya ukaguzi wa madini?
Shahidi:Sina.
Wakili:Timu yenu ilikuwa inawajibika kwa nani?
Shahidi:Gavana(Marehemu Daud Ballali).
Wakili: Unafahamu mchakato mzima ulitakiwa kusimamiwa na BoT kwa niabaya ya serikali?
Shahidi:Siwezi kujua.
Wakili:Juzi ulisema Gavana alisaini mkataba mkataba wa serikali na kampuni hiyo, mwingine aliyesaini huo mkataba ni nani?
Shahidi:Katibu wa BoT, Bosco Kimela na huyu Edwin Frolence alisaini kwaniabaya kampuni hiyo na mkataba ulisainiwa Juni 14 mwaka 2003.
Wakili:Timu yenu ya majadiliano ndiyo ilipelekea mkataba huo kusainiwa?
Shahidi:Ndiyo.
Wakili:Timu yenu ilikuwa huru kufanyakazi na wala haikuingiliwa na mtu?
Shahidi:sikumbuki.
Wakili:Hawa washitakiwa walishawahi kuingilia timu yenu?
Shahidi:Sijawahi kuwashuhudia wakiingilia timu yetu.
Wakili:Mkataba uliosaini ni matokeo ya timu yenu, Je ndiyo ulioweka kipengele cha kodi?
Shahidi:Siyo kwasababu kipengele katika timu yetu tulikiwa kando na pia isingewezekana kwani waziri hakuwa ameishatoa msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo.
Wakili:Timu yenu ndiyo iliyopitisha ada ya kampuni hiyo iwe asilimia 1.9 na mkaiweka kwenye ule mkataba?
Shahidi:Ndiyo tuliweka ada hiyo.
Wakili:Unafahamu Juni 4 mwaka 2003 timu yenu ilimjulisha Yona kwamba suala la ada limeishamalizika na barua hiyo iliandikwa na Gavana?
Shahidi:Hilo silifahamu.
Wakili:Nikikwambia barua hiyo ipo?
Shahidi:Sibishi.
Waliki:Ulisema waziri ndiye mwenye mamlaka ya mwisho ya kutoa msamaha wa kodi sasa kwanini wewe ulipeleka barua TRA kuomba ushauri?
Shahidi:Ieleweke hakuna mahala popote panapomlazimisha waziri wa Fedha aombe ushauri wa msamaha wa kodi kwa kampuni yoyote kwa TRA.
Wakili:Mkataba huo ulikuwa unasemaje?
Shahidi:Ulisema Alex Stewart itasamehewa kodi zote.
Wakili:Jukumu la Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwenye matangazo ya serikali nini?
Shahidi:Ni kuakikisha matangazo ya serikali linakubalika kisheria.
Kesi hiyo iliahirishwa hadi Desemba 15-18 mwaka huu, itakapokuja kwa ajili ya shahidi wa tatu wa upande wa mashitaka kuanza kutoa ushahidi wake.
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Novemba 6,2009



